JENGO la Shirika la Bima la Taifa, mkoani Kilimanjaro (NIC), juzi lilinusurika kuteketea kwa moto baada ya moto mkubwa kuibuka katika moja ya Vyumba vya ofisi zake na kuteketeza baadhi ya nyaraka muhimu kabla ya zima moto kufika na kuuzima kabla haujasababisha madhara makubwa.
![]()
Kwa mujibu wa maelezo kutoka kwa mashuhuda wakiwemo baadhi ya wafanyakazi wa shirika hilo, lililoko katika Jengo namba 2021, mtaa wa TRA, Manispaa ya Moshi, mkoani hapa, moto huo ulianzia katika moja ya vyumba vinavyotumika kuhifadhia nyaraka za Bima.![]() |
Baadhi ya maeneo ya ofisi katika Jengo hilo yaliyoathirika na moto huo |
TAIFA LETU.com ilifika katika eneo la tukio na kukuta sehemu kubwa ya moto huo ukiwa umeshazimwa kutokana na juhudi za pamoja ya wafanyakazi wa Shirika hilo kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kitengo cha zimamoto, ambao tofauti ilivyozoeleka walifanikiwa kuwahi kufika katika eneo la tukio.
![]() |
Polisi wakikagua Baadhi ya maeneo ya ofisi katika Jengo hilo yaliyoathirika na moto huo |
Akizungumza na gazeti hili kuhusu chanzo cha moto huo, Meneja wa shirika hilo mkoani Kilimanjaro, John Mdenye alisema chanzo cha moto huo haujafahamika bado na kuongeza kuwa alipata taarifa kutoka kwa katibu wake kuhusu kuonekana kwa Moshi ikitokea katika moja ya Stoo za Shirika hilo.
![]() |
Meneja wa NIC mkoani Kilimanjaro, John Mdenye akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu chanzo cha moto huo |
“Nilikuwa Ofisini tangu saa mbili asubuhi, majira ya saa sita hivi, Principle wangu alikuja na kunieleza kuwa kuna moshi katika stoo yetu ya kuhifadhia faili za bima, baada ya kama dakika 10 kuliibuka moto mkubwa kutokea maeneo hayo, haraka niliwasiliana na zima moto ambao walikuja kutoa msaada,” alisema Mdenye.
![]() |
Mmoja wa Wafanyakazi akizungumza na Waaandishi wa Habari |
Aidha Meneja huyo alisema mpaka sasa haijafamika moto huo utakuwa umesababishwa na nini japo wanahisi huenda moto huo utakuwa umeanzia katika ngazi za kupanda juu ambako kuna nyumba ya mpangaji mmoja ambaye ni mfanyakazi wa Mamlaka ya Mapato (TRA).
![]() |
Gari la zimamoto likiondoka katika eneo la Jengo la Shirika la Bima ya Taifa, lililowaka moto |
Alisema hisia hizo hata hivyo hazitoi uthibitisho wa moto kuanzia katika nyumba ya mpangaji huyo kwani kilichoonekana mpaka sasa ni kuwepo kwa mtungi wa gesi katika sehemu ya chini ya ngazi hizo hivyo kutoa wasiwasi huenda mpangaji huyo alikuwa anapikia hapo kutokana na sheria katika mkataba kutomruhusu kupika katika nyumba yake iliyoko ghorofani kwa usalama wa ofisi za bima zilizoko chini.
![]()
Mpaka sasa haijafahamika kiasi cha thamani ya mali iliyoharibiwa kutokana na moto huo japo hadi mwandishi wa gazeti hili anaondoka katika eneo la tukio, mali iliyoripotiwa kuharibika ni faili zote za bima zilizoteketea katika moto huo, kompyuta mbili moja ikiwa ni kompyuta mpakato ya Meneja huyo.