
Steve alikutana na wasanii hao hivi karibuni jijini Dar es Salaam ambako aliwasisitiza kujiheshimu katika mavazi pindi wanapocheza filamu.
“Nataka heshima irudi katika filamu, si kila mtu anakuwa anacheza filamu kwa kuvaa mavazi ya kujidhalilisha ya nusu utupu,” alisema Steve.
Aliongeza kuwa ana mkakati wa kuleta mapinduzi katika Bongo Movie ili kurudisha heshima.
“Nimewaambia haiwezekani mama yuko nyumbani eti kavaa kimini na blauzi ambayo mwili wote na kifua kikionekana.
Wanawake wa Kitanzania tunawajua na kwa ushahidi hata wao wanatambua, ila wanaleta ukaidi usiokuwa na maana tu,” alisema Steve na kuongeza kwamba, kwa kuwa filamu zetu zinapendwa na zinauzwa mbali, wasanii wa kike wanapaswa kuwa mabalozi wema ndani na nje ya nchi, kwa kumjengea heshima mwanamke wa Kitanzania.
Alifafanua kuwa kama mtu yuko katika ‘sini’ ya kucheza na nguo za aina, hiyo hakuna shida, avae lakini haiwezekani kila sehemu waigizaji wa kike wawe wamevaa nguo za kujibana na fupi zinazowachoresha.